Klabu ya US Goree inayoshiriki Ligi Kuu nchini Senegal imeandika barua rasmi ya kusikitishwa na kitendo cha Azam ya Tanzania kumsainisha nyota wa timu hiyo, Alassane Diao mwenye mkataba nao.
Azam juzi ilimtambulisha nyota huyo na kumpa mkataba wa miaka miwili jambo lililowashtua Goree kwa kile walichoeleza kutofurahishwa na kilichofanyika kwani taratibu za usajili hazikufuatwa.
"Kwa kukumbushana US Goree inapenda kudokeza kuwa mchezaji Alassane Diao bado ana mkataba na klabu yetu na hakuna mazungumzo yoyote yaliyoanzishwa na Azam kuhusu mwelekeo wa kumuachia," ilisomeka taarifa hiyo.
Aidha taarifa hiyo ilieleza Diao hawezi kufuzu wala kucheza katika klabu nyingine nchini Senegal au kimataifa kabla ya kumalizika kwa mkataba wake mahakamani ambao bado umesalia na timu hiyo.
"Kwa kuheshimu maandishi yanayosimamia soka, US Goree inasisitiza dhamira yake ya kufuata sheria za uhamisho zilizowekwa na FIFA na kuhakikisha maslahi ya klabu na wachezaji wake chini ya mkataba."
Usajili wa nyota huyo ulihitimisha wachezaji wanne waliosajiliwa kwa ajili ya msimu ujao huku wengine ni Feisal Salum 'Fei Toto' (Yanga), Gibril Sillah (Raja Casablanca) na Cheikh Sidibe kutoka Teungueth.