Taifa Stars imeitoa kimasomaso Tanzania baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 ugenini dhidi ya Guinea katika mechi ya kuwania kufuzu fainali za mataifa ya Afrika (Afcon) 2025 iliyochezwa katika Uwanja wa Charles Konan Banny, Yamoussoukro, Ivory Coast.
Mabao ya mchezo huo yamefungwa na Feisal Salum ‘Fei Toto’ na Mudathir Yahya kwa Stars huku Mohamed Bayo akiifungia Guinea.
Matokeo hayo ya leo yameifanya Taifa Stars kusogea hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa kundi H ikiwa na pointi nne huku kinara ikiwa ni DR Congo yenye pointi sita.
Taifa Stars itarejea uwanjani Oktoba 6 kwa kukabiliana na DR Congo ugenini na kisha timu hizo zitarudiana Oktoba 14 katika Uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es Salaam.
Timu mbili zitakazomaliza zikiwa juu ya msimamo wa kundi H zitafuzu fainali za Afcon ambazo zitafanyika Morocco mwakani.