Kikosi cha timu ya Taifa Tanzania 'Taifa Stars' kinatarajia kuondoka nchini leo majira ya saa kumi jioni kuelekea Kenya katika mchezo wa marudiano.
Katika mechi ya kwanza kufuzu CHAN, Stars walitoka sare ya 0-0 dhidi ya Kenya na mchezo wa marudiano utapigwa Agosti 4 nchini Kenya.
Akizungumza na Mwanaspoti,Meneja wa timu hiyo Nadir Haroub alisema maandalizi yapo vizuri na yeye anatangulia ili kwenda kuweka kila kitu sawa.
"Mimi nawahi kuondoka muda huu kwasababu kuna vitu natakiwa kwenda kuweka sawa, nazani mpaka saa kumi nao wataanza safari ya kuja," alisema.
Wachezaji wanaotarajiwa kuondoka leo ni 20, huku mshambuliaji Ibrahim Ajib akiachwa kutokana na maumivu ya mguu yanayomkabili.
Katika mchezo huo Stars wanahitaji ushindi au sare ya magoli ndio waweze kuvuka kwenda hatua inayofuata, lakini kama wakitoka sare ya bila kufungana watapigiana mikwaju ya penalti.