Mchezaji wa zamani wa timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' pamoja na vilabu vya Yanga na Simba, Bakari Malima 'Jembe Ulaya' amesema kuwa, wapo baadhi ya wachezaji wa yanga ambao uwezo wao umefika mwisho, hivyo iwapo klabu hiyo inataka kufanya vizuri zaidi kimataifa, wanapaswa kuwaondoa na kuleta wachezaji wenye ubora zaidi yao.
Jembe Ulaya amesema kuwa, wachezaji hao wana uwezo mzuri wa kucheza na kushinda kwa Ligi ya ndani lakini si kwa michuano ya kimataifa ambayo inahitaji wachezaji bora na wenye uzoefu mkubwa na michuano hivyo.
"Kuna baadhi ya mapengo yanaonekana Yanga, baadhi ya wachezaji wanaonyesha kabisa hawana uwezo tena wa kuisaidia Yanga. Kwa Ligi ya ndani wako vizuri ila kule CAFCL inatakiwa quality kubwa.
"Tanzania tumeanza kuteka soka la Afrika, tunapaswa tuachane na wachezaji wa milioni 50 na milioni 30, tulete wachezaji wa milioni 100, au milioni 150, kwa vyovyote akija hapa atatupa kikubwa zaidi," amesema Jembe Ulaya.