Klabu ya Ligi Kuu ya NBC ya Singida Fountain Gate FC imefungiwa kusajili mpaka itakapomlipa mchezaji wake, Nicholas Gyan.
Uamuzi huo umefanywa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) baada ya mchezaji huyo kushinda kesi ya madai dhidi ya klabu hiyo.
Mchezaji huyo raia wa Ghana alifungua kesi FIFA akidai malipo ya ada ya usajili (sign on fee) na malimbikizo ya mshahara.
Klabu hiyo ilitakiwa iwe imemlipa ndani ya siku 45 tangu uamuzi huo ulipotolewa, lakini haikutekeleza hukumu hiyo.
Wakati FIFA imeifungia klabu hiyo kufanya uhamisho wa wachezaji kimataifa, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeifungia kufanya uhamisho wa ndani.