Dar es Salaam. Baada ya wachezaji wa Kitanzania, Ramadhani Singano ‘Messi’ na Eliud Ambokile kuonja utamu wa Ligi Kuu DR Congo wakiwa na TP Mazembe, wamezungumzia ugumu wa Ligi hiyo, wakilinganisha na Ligi Kuu Tanzania Bara.
Singano aliyeanza katika mchezo uliopita dhidi ya Lubumbashi Sport, amesema utofauti aliouona ni kwamba kila mchezo kule huwa na uzito wa namna yake tofauti na Tanzania ambapo uzito ni katika michezo mikubwa pekee.
“Kila timu inaonekana kuwa vizuri. Nilivyoona nimepangwa kuwa nitaanza kikosi cha kwanza nilifurahi kwa sababu ni nafasi ambayo nilikuwa naisuburi kwa hamu, mechi ilikuwa ngumu, lakini kikubwa tulipata pointi tatu,” alisema Singano.
Ambokile alisema licha ya kutokuwa mshambuliaji wa kutegemewa katika kikosi hicho, anauona mwanzo wake kama ilivyokuwa Mbeya City.
Ambokile alisema alikuwa akikosa nafasi hadi katika mazoezi akiwa Mbeya City kutokana kukosa nafasi kikosi hicho, lakini muda uliongea, akawa mmoja wa wachezaji muhimu.
“Taratibu watanielewa kikubwa ni uvumilivu kwa sababu hata Mbeya City sikuwa na nafasi ya kucheza kikosi cha kwanza, lakini kujituma kwangu kulileta wepesi. Kuna mambo najifunza kwa wale ambao ni chaguo la kwanza,” alisema Ambokile.
Pia Soma
- Simbu, Huche na Sulle washindwa kung’ara Qatar
- Bondia Mtanzania achapwa raundi ya kwanza Russia
- Molinga kuibeba tena Yanga ikiikabili Coastal Union?