Dar es Salaam. Kocha wa Simba, Patrick Aussems amesema kambi ya timu hiyo nchini Afrika Kusini ilikuwa na mafanikio.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Aussems alisema ana matumaini mafunzo waliyopata wachezaji yatakuwa chachu ya kupata matokeo mazuri katika mashindano ya msimu ujao.
“Ingawa niliondokewa na wachezaji wangu waliokwenda kujiunga na kambi ya Taifa Stars, lakini naamini mafunzo waliyopata yatakuwa na tija,” alisema Aussems.
Alisema amejiandaa kutoa ushindani katika mashindano ya msimu ujao kwa kuwa ana kikosi bora chenye wachezaji wanaojituma.
Simba imerejea baada ya kucheza mechi nne za kirafiki ilianza kwa kuilaza Orbret mabao 4-0, iliichapa Platinum Stars 4-1, ilitoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Township Rollers.
Simba ilihitimisha ziara ya mafunzo kwa kutoka sare ya bao 1-1 dhidi kigogo cha soka Orlando Pirates.
Pia Soma
- Kindoki ampisha Mkongo Yanga
- Straika Mpya Yanga asaini rasmi
- Evra: Nilificha mfupa mguuni nikiwa uwanjani
Agosti 3, wachezaji wa Simba watatembelea Hospitali ya Ocean Road ambako watatoa misaada kwa wagonjwa ikiwa ni maadhimisho ya sherehe hizo.
Simba inatarajiwa kuanza kampeni ya kuwania ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kuvaana na UD Songo ya Msumbiji, Agosti 10 ambapo itakuwa ugenini.