JAPO imetolewa katika michuano ya kimataifa, licha ya ushindi wa mabao 3-0 iliyopata mbele ya Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini, Simba imeendeleza rekodi yake ya nyumbani kwa leo kutimiza jumla ya miezi 99 bila kupoteza ikiwa jijini Da es Salaam. Simba ilipata ushindi huo kwenye mchezo wa marudiano wa robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika 2020-2021, lakini imetoka kwa ushindi wa mabao 4-0 iliyopata Kaizer ikiwa kwao na kufanya itinge nusu fainali kwa jumla ya mabao 4-3.
Hata hivyo, licha ya kutolewa Simba imeendeleza rekodi katika michuano hiyo, ikiwa uwanja wake wa nyumbani katika michuano ya kimataifa kwani leo imetimiza jumla ya miezi 99 bila kupoteza katika ardhi yao. Miezi hiyo ni sawa na siku 3016 au miaka nane na miezi mitatu na siku tani, tangu ilipopoteza mechi yao ya mwisho nyumbani dhidi ya Recreativo do Libolo ya Angola. Simba ilicharazwa bao 1-0 na Waangola katika mechi ya mkondo wa kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika iliyopigwa Februari 17, 2013 kabla ya kwenda kulala 4-0 ugenini waliporudiana Machi 3. Katika mchezo wa leo uliomalizika muda mfupi uliopita, mabao ya Simba yalifungwa na nahodha John Bocco aliyetupia mawili na jingine likizamishwa kimiani na kiungo Mzambia Clatous Chama.
Kaizer sasa wanaungana na watetezi Al Ahly ya Misri iliyolazimisha sare ya 1-1 ugenini dhidi ya Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini ambayo ilikubali kichapo cha 2-0 kwenye mechi yao ya kwanza. Timu nyingine mbili za kutinga nusu fainali zitafahamika usiku huu wakati timu za Wydad Cadablanca itakaporudiana na MC Alger na Esperance ya Tunisia itakapoialika majirani wao wa CR Belouizdad ya Algeria.