Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Simba yafuata mbadala wa Inonga Asec Mimosas, ni beki wa kazi

Tra Bi Tra Ges (5).jpeg Beki wa kati wa Asec Mimosas ya Ivory Coast, Anthony Tra Bi Tra.

Tue, 18 Jun 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wakati Mwekezaji, Rais wa Heshima na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba, Mohamed 'Mo' Dewji, akitangaza wajumbe sita upande wake, zikiwamo sura tatu mpya, klabu hiyo imetajwa kuanzisha mazungumzo na beki wa kati wa Asec Mimosas ya Ivory Coast, Anthony Tra Bi Tra ili kuziba nafasi ya Henock Inonga ambaye taarifa zinaeleza ameshamalizana na FAR Rabat ya Morocco.

Akizungumza juzi usiku, Mo, pamoja na mambo mengine, aliwatangaza wajumbe sita upande wa mwekezaji kuziba nafasi za wale waliojiuzulu hivi karibuni, watatu wakiwa wapya akiwamo mjumbe wa zamani wa bodi hiyo na Ofisa Mtendaji Mkuu, Crescentius Magori.

Wengine ni Mohamed Nassor na Hussein Kita, huku watatu pia wakirejeshwa ambao ni Salim Abdallah 'Try Again' ambaye alimtangaza siku chache zilizopita, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, Rashid Shangazi na Zulfikar Chandoo.

Sura mbili ambazo hazipo katika bodi hiyo ni Dk. Rafael Chegeni na Hamza Johari, ambao kwa mujibu wa Mo wameomba wasijumuishwe kutokana na kutingwa na majukumu mengine.

"Johari, ameomba apumzike kwa ajili ya majukumu ya kikazi, lakini nimemuomba aingie kwenye Baraza la Ushauri, na Rafael Chegeni, ameomba apumzike kwenye Bodi ya Simba, maana ana bodi nyingi anazohudumu kwa sasa, ila ataendelea kuwa mshauri na mtu muhimu sana katika familia ya Simba," alisema Mo, wakati wa kutangaza wajumbe hao.

Kabla ya kurejeshwa ujumbe wa bodi, Magori alikuwa ni Mshauri Binafsi wa Mo kwenye masuala ya michezo, na kabla ya hapo aliwahi kuhudumu nafasi ya Ofisa Mtendaji Mkuu wa klabu, ambapo pia alikuwa mjumbe wa bodi upande wa mwekezaji.

Mo pia aliipongeza timu ya Simba Queens kwa kutwaa ubingwa wa Tanzania Bara kwa upande wanawake, akiahidi kukuta nao kabla ya msimu kuanza na kuwapa zawadi.

"Nichukue nafasi hii kuipongeza timu yetu ya Simba Queens, kwa kutwaa ubingwa wa Tanzania Bara, muda si mrefu nitapata muda wa kukutana nao kabla ya msimu kuanza, nitawapa zawadi yangu binafsi kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kupeperusha bendera ya Simba, hongereni sana Simba Queens," alisema.

Aliwapongeza pia vijana wa Simba chini ya miaka 20 kwa kufikia hatua ya nusu fainali ya ligi hiyo, na chini ya miaka 17 ambayo inafanya vema katika ligi ya vijana wa umri huo.

Wakati hayo yakiendelea, klabu hiyo inadaiwa kuanzisha mazungumzo na beki wa kati Asec Mimosas, Tra Bi Tra ili kuziba nafasi ya Inonga.

Habari kutoka ndani ya klabu hiyo zinaeleza kuwa mazungumzo yameanza ingawa bado hayajafika mwisho.

"Tuna tatizo la beki mkakamavu. Tangu alipoondoka Joash Onyango tumeonekana kuyumba sana, Fondoh Che Malone na Inonga wanaonekana wana aina moja ya uchezaji na hawatumii nguvu, na siyo wagonganaji, hivyo mastraika hawaogopi, huyu anayefuatiliwa yupo vizuri kote kote, ana akili ya mpira na mpambanaji," alisema mtoa taarifa.

Taarifa kutoka ndani ya klabu hiyo zinaeleza kuwa tayari dili la Inonga kwenda FAR Rabat limekamilika, ambapo kuna makubaliano yamefanyika baina ya pande zote tatu na huenda akatua kwa klabu yake hiyo mpya hivi karibuni.

Wakati huo huo Klabu ya Simba imetangaza rasmi nahodha wao, John Bocco, hatakuwa sehemu ya kikosi chao msimu ujao, lakini pia ikiweka wazi kuwa imempa majukumu mapya ya kuwa kocha wa timu ya vijana ya chini ya umri wa miaka 17.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live