Kila mshabiki wa mpira wa miguu nchini, anajua Jumamosi mechi ya Yanga na Simba Ligi Kuu Tanzania Bara Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam itakuwa ngumu na isiyotabirika.
Hata Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga SC, Ali Kamwe naye anajua hilo jambo kwamba mechi ngumu, lakini leo katika mahojiano, Kamwe amesema kama Simba watajichanganya siku hiyo, uwezekano wa kuwafunga mabao 7-0 au 8 ni mkubwa.
Amesema ikitokea wachezaji wa Yanga SC wameamka vizuri, na wale wa Simba wameamka na mawazo yao, sio dhambi kuwanyuka goli saba, nane na wala halitakuwa kosa.
Amesema kuelekea mchezo huo lengo lao ni kusaka pointi tatu ila wana uchu wa kufunga.
“Ikitokea wakajichanganya, nafasi zile za kufikia goli saba, nane nakwambia nafasi kwa maana Aziz Ki anaweza kufunga goli mbili, Max anaweza kufunga goli mbili, Pacome anaweza kufunga, Musonda anaweza kufunga, mtambo wa magoli Mudathir anaweza kufunga, Mzize anaweza kufunga, Guede anaweza kufunga, unakosaje goli saba?" anahoji Kwamwe.
Kamwe ameshauri watangazaji wa mchezo huo kuwekewa maji mengi maana kama ikitokea kipigo hicho basi huenda makoo yao yatakauka.