Mchezo wa Dabi ya Mzizima kati ya Simba na Azam kuanza, mashabiki wameitika uwanjani hapo wakijitokeza kwa wingi, huku nusu ya Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza ukiwa tayari umejaa.
Simba na Azam zitaumana saa 10:00 Alasiri katika Uwanja huo kwenye mchezo wa Ligi kuu, ukiwa ni mchezo wa 30 kuzikutanisha timu hizo na katika michezo 29 iliyopita Simba imeshinda mara 12, Azam mechi nane na sare tisa.
Viingilio vya mchezo huo ni Sh20,000 jukwaa kuu, Sh10,000 jukwaa la VIP B na Sh5,000 mzunguko.
Mapema leo saa 6 mchana Simba ambayo ni mwenyeji wa mchezo huo imetangaza kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii kuwa tiketi za jukwaa kuu (VIP A) zimekwisha na jukwaa hilo lina uwezo wa kubeba mashabiki zaidi ya 500.
Hata hivyo, misururu mirefu ya mashabiki bado imeendelea kushuhudiwa nje ya uwanja huo wakisaka tiketi za kuingia uwanjani huku wengine wakiwa kwenye foleni za kuingia getini.
Mmoja wa mashabiki wa Simba jijini hapa, Aneth Mikomangwa, amesema wamejitokeza kwa wingi kuitazama timu yao ikivuna ushindi dhidi ya Azam kwani wana imani kubwa na kikosi chao kwa sasa kutokana na matokeo mazuri wanayoyapata, huku akitamba kwamba Azam FC atakufa mabao 3-0 ndani ya CCM Kirumba, Mwanza.