Vilabu vya Simba na Yanga vimeungana na Watanzania wote kutoa salamu za pole kufuatia ajali ya ndege ya Precision Air iliyotokea mkoani Kagera katika Ziwa Victoria.
Ajali hiyo imehusisha ndege aina ya ATR 42-500 ambayo ilianguka katika Ziwa Victoria, mita 100 kutoka kwenye uwanja wa ndege wa Bukoba.
Hadi sasa jumla ya watu 19 wamefariki dunia huku wengine wakiokolewa wakiwa na majeraha mbalimbali na tayari wanaendelea kupatiwa matibabu mkoani humo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Novemba 6, 2022 na Idara ya Habari na Mawasiliano ya Klabu ya Yanga, uongozi umepokea kwa masikitiko taarifa za ajali hiyo huku wakimwomba Mungu awasaidie majeruhi wote.
"Uongozi wa Klabu ya Yanga SC umepokea kwa masikitiko taarifa ya ajali ya ndege ya Shirika la Precision katika Ziwa Victoria mkoani Kagera.
"Tunatoa salamu zetu za pole kwa wote walioathirika na ajali hii. Mwenyezi Mungu awasaidie majeruhi wote wapone haraka," inaeleza taarifa hiyo ya Yanga.
Kwa upande wao, Simba katika taarifa yao imeeleza kwamba inatoa pole kwa wote walioathirika kwenye ajali hiyo, ndugu, jamaa na uongozi wote wa Precision.
"Tunawaombea majeruhi wote waweze kupona kwa haraka na kurejea katika shughuli zao. Simba tunatoa pole kwa wote walioathirika kwenye ajali hiyo, ndugu, jamaa na uongozi wa Precision," inaeleza taarifa ya Simba.
Mbali na vilabu vya Simba na Yanga, Rais Samia naye ametuma salamu za pole kwa Watanzania na kuwataka kuwa watulivu wakati jitihada za uokoaji zikifanyika.
Waziri Mkuu, Kassimu Majaliwa amewasili mkoani Kagera na kutangaza kuwa watu 19 wamekufa katika ajali hiyo ya ndege inayoelezwa kwamba ilikuwa na abiria 43.