Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Simba Queens yaponzwa na jina

SIMBA QUEENS.png Simba Queens yaponzwa na jina

Tue, 14 Sep 2021 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

SIMBA Queens imerejea nchini huku ikiwa imekwama kutimiza ndoto zao za kubeba ubingwa wa Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) ili kukata tiketi ya kushiriki Klabu Bingwa Afrika, huku kocha wake Hababuu Ali Omary akisema waliponzwa na ukubwa na mafanikio ya kaka zao kwenye michuano ya kimataifa.

Simba ilimaliza wa nne kwa kufungwa mabao 2-1 na Lady Dove ya Uganda kwenye mchezo wa kusaka mshindi wa tatu, baada ya awali kufurushwa nusu fainali na Vihiga Queens ya Kenya iliyotwaa ubingwa wa michuano hiyo iliyochezwa kwa mara ya kwanza jijini Nairobi.

Kocha Hababuu alisema amefurahishwa na mafanikio ya timu yake licha ya kushindwa kutimiza malengo, lakini akikiri mafanikio ya timu ya wanaume iliwapa kazi kubwa kwenye michuano hiyo kwa kukamiwa hasa hatua zile za mtoano.

“Tulipofikia sio haba, nawapongeza wachezaji wangu na kilichobaki twende kwenye ligi tukafanye vizuri zaidi ila hata mwakani tutakapopata nafasi tuje tufanye bora zaidi ya msimu huu.”

“Watu wanatuchukulia ni wakubwa kutokana na Simba ya kiume inavyofanya, ila wanatakiwa watambue sisi bado tunakua, lakini hata ukiangalia Simba ya wanaume imesafiri na ndege kwenda Arusha katika maandalizi ya msimu mpya ila sisi tumekuja na basi Kenya unaoana utofauti.”

Kocha msaidizi wa timu ya taifa ya Wanawake, Edna Lema alipongeza waandaji wa michuano hiyo ya wanawake na kutoa wito kwa klabu za Ligi Kuu ya Wanawake (WPL) nchini kujijenga vyema ili katika misimu inayokuja waweze kufanya vizuri zaidi.

“Michuano ilikuwa na ushindani mkubwa sana na tuwapongeze waandaaji kwani itasaidia kuukuza soka la wanawake Afrika juhudi kubwa ni klabu kuandaa timu za kiushindani ili kuweza kuonyesha upinzani mkubwa kama walivyofanya Simba mwaka huu,” alisema Lema.

Naye kocha mkuu wa Mlandizi Queens, Hussein Kioma ametoa wito kwa wadau kujitokeza kudhamini ligi hii kwani kuwepo kwa pesa ni chachu ya kuendeleza mchezo. “Wazazi pia ni muda sasa wa kuwaruhusu watoto wao wa kike kucheza mpira kwa nao ni ajira na mtoto anaweza kuendesha maisha yake kupitia soka,” alisema Kioma.

Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz