Nchini Uturuki mchezo wa soka wa Derby kati ya klabu ya Goztepe FC na Atlay FC ulilazimika kuahirishwa baada ya shabiki kuvamia uwanjani na kumtandika golikipa wa Atlay kwa kutumia mlingoti wa kibendera cha kona.
Awali mchezo huo wa mahasimu hao ulisimamishwa kwa muda baada fataki kulipuka na kusababisha shabiki mmoja kujeruhiwa hali iliyopelekea gari la Wagonjwa (ambulance) kuingia uwanjani.
Wakati shabiki akipokea huduma ya kwanza kabla ya mchezo kuendelea ndipo shabiki mwingine alipoingia uwanjani na kung'oa mlingoti wa kibendera cha kona na kumchapa golikipa, Ozan Evrim Ozenc mara mbili kabla ya kuokolewa na wachezaji wenzake.
Kwa mujibu wa ripoti golikipa huyo alitokwa na damu nyingi na kulazimika kukimbizwa hospitalini ambako anaendelea kujitambua licha ya kupata jeraha kubwa kichwani.