Shabiki maarufu wa Klabu ya Simba, anayefahamika kwa jina la Mchome amesema kuwa Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Klabu hiyo, Ahmed Ally anapaswa kujifunza namna ya kufanya kazi yake kama anavyofanya Ofisa habari wa Yanga, Ally Kamwe.
Mchome amesema kuwa, Kamwe amekuwa akifanya hamasa zenye mafanikio na kwa maslahi ya klabu tofauti na Ahmed ambaye amedai kuwa anafanya mambo kwa maslahi yake binafsi huku akimchana kuwa aache maringo.
“Ahmed Ally ana vitu vingi vya kujifunza kutoka kwa Ally Kamwe. Kamwe anafanya vitu kwa maslahi ya timu lakini Ahmed anafanya kwa maslahi yake binafsi.
“Ukimsikiliza Ahmed akizungumza, hazungumzi kitimu wala kisoka, anazungumza yeye kama yeye. Ajifunze kuwa na mapenzi na timu yake, afanye kitu kwa niaba ya Wanasimba, Wanasimba tunakutegema msemaji wetu, jifunze hamasa kwa Kamwe, jifunze swaga.
“Digrii imeenda Yanga, ubunifu wa kutosha, Kamwe ni bwana mdogo ambaye hana maringo kama wewe, havimbi kama wewe. Mimi navuta picha iwapo Ahmed Ally angekuwa msemaji wa Yanga, halafu Yanga hii, ingekuwaje? Si dunia ingejaa bahari hii?,” amesema Mchome.