Mabosi wa Omonia Nicosia ya Cyprus wameripotiwa kuvalia njuga dili la kumnasa nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta ambaye kwa sasa anaonekana kutokuwa kwenye mipango ya kocha wa PAOK, Razvan Lucescu.
Samatta ambaye ana mkataba wa kuichezea miamba hiyo ya soka la Ugiriki hadi Juni 30, 2025, awali alikuwa katika rada za Al Kholood iliyopanda Ligi Daraja la Pili Saudi Arabia ambako baadhi ya mastaa wa soka Ulaya wanakimbilia.
Kwa mujibu wa taarifa inaelezwa kuwa viongozi wa PAOK wameanza mazungumzo na Omonia Nicosia na inaelezwa vigogo hao wapo tayari kulipa mara mbili ya kile ambacho nahodha huyo wa Taifa Stars anavuna huko Ugiriki.
Mmoja wa marafiki wa karibu wa Samatta amethibitisha hilo akisema mshambuliaji huyo anaweza kuondoka muda wowote pamoja na kwamba msimu uliopita alitwaa ubingwa wa Ligi Kuu akiwa na timu hiyo.