Ofisa Habari wa klabu ya Geita Gold Hemed Kivuyo ameibuka na kutoa ufafanuzi juu ya kile kinachoendelea kuhusu Sakata la mchezaji wa klabu hiyo na mfungaji bora wa Ligi Kuu ya NBC Msimu uliopita George Mpole.
Kivuyo amebainisha kuwa Mpole aliondoka klabuni hapo bila taarifa kwa uongozi wa klabu hiyo na hata hoja yake ya kuwa anauguza majeraha ameisikia kwenye vyombo vya Habari.
Mpole amekuwa nje ya kikosi cha Geita Gold FC kwa muda mrefu sasa huku kukiwa na taarifa amkanganyiko ambapo yeye binafsi anadai kuwa anauguza majeraha yake baada ya klabu ya Geita Gold kumtelekeza na kutomsaidia kupata matibabu.
Aidha Mpole amenukuliwa akilalamika juu ya kukatwa mshahara wake wa mwezi kutokana na kutoonekana kambini wakati yeye akitoa sababu ya kuwa anauguza majeraha.
Sakata la Mpole kutokuwepo kwenye kikosi cha Geita Gold kilianza tangu afanyiwe mabadiliko katika pambano la Ligi Kuu ya NBC dhidi ya Coastal Union ya mkoani Tanga.