Mchambuzi wa soka Bongo, Jemedari Said amesema safari ya Yanga SC kwenye mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika inaishia Robo Fainali na si vinginevyo.
Jemedari amesema, si Yanga tu hata Simba SC hawana uhakika wa kutoboa Nusu Fainali licha ya wapinzani wao Al Ahly kuonekana kupungua kiwango chao.
"Huwezi kuona sasa hivi Mamelodi anamfikiria Yanga kama ambavyo Yanga sasa hivi anamfikiria Mamelodi. Mamelodi yeye anajua akikutana na Yanga atamfunga basi lakini Yanga sasa hivi anawaza anajua anakutana na timu kubwa na ngumu.
"Ndio maana hata Rais wa Yanga Injinia Hersi Said alipoulizwa maoni yake alisema timu anazoona zinaweza kufika fainali na kubeba ubingwa ni Mamelodi na Al Ahly, amesema hivyo na yeye ni Rais wa Yanga kwa nini asiitaje Yanga?
"Hakuitaja Yanga sababu anajua hana wachezaji wenye ubora wa kufanana na Mamelodi. Hata Simba, pamoja na kwamba wanakutana na Al Ahly ambayo kiwango kimeshuka lakini hata wao wanajua wanakutana na timu ngumu ambayo inaweza kuwatoa," alisema Jemedari.