KIUNGO wa Manchester United, Paul Pogba ametajwa kuwa huenda akahamia kwa miamba ya soka ya Ufaransa, Paris Saint Germain, ambapo inaelezwa kuwa amekutana na Mkurugenzi wa Michezo wa PSG, Leonardo Nascimento de Araújo katika kipindi ambacho mkataba wake na United ukiwa mwishoni kumalizika.
Inafahamika kuwa kiungo huyo anataka kujiunga na wababe hao wa Ufaransa mara tu baada ya mkataba wake na United kumalizika huku ikielezwa kuwa hana mpango wa kusaini mkataba mpya na United.
Hatma ya Pogba ndani ya United mpaka sasa haijajulikana, ambapo nyota huyo ameweka wazi kuwa hana furaha ndani ya kikosi hicho kutokana na kushindwa kufikia malengo yake ya kuwania mataji aliyokuwa akiyatarajia wakati alipojiunga nao akitokea Juventus kwa ada ya uhamisho ya pauni milioni 89 mwaka 2016.
Timu mbalimbali kubwa za Ulaya zimeonyesha nia ya kumsajili Pogba zikiwemo Real Madrid na Juventus lakini bado PSG inaonekana kupewa nafasi kubwa ya kumchukua staa huyo.