Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Sababu ya Mpole kusaini Pamba Jiji

George Mpole Pamba FC George Mpole

Sun, 11 Aug 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Baada ya dili la kujiunga na Yanga kukwama, kisha kuwepo kwa taarifa kwamba alikuwa mbioni kwenda nje ya nchi, straika George Mpole jana alionekana akiwa na kikosi cha Pamba Jiji katika mechi ya kirafiki dhidi ya Vital'O ya Burundi na kufichua sababu za kujiunga na timu hiyo iliyopanda Ligi Kuu msimu huu.

Mfungaji Bora huo wa Ligi Kuu msimu wa 2021-2022, ameliambia Mwanaspoti kuwa, sababu za kusaini miezi sita Pamba ni kutaka kujipanga ili kusubiri madili mapya dirisha la usajili litakapofunguliwa.

Mpole alisema hakuwa na namna ya kusaini timu zilizokuwa zinamhitaji, kutokana na kuchelewa kupata barua kutoka FC Lupopo ya Kongo, ila kwa sasa anajipa muda anaona kila kitu kitakwenda kuwa sawa.

"Nimeamua kusaini Pamba kwa mkataba wa miezi sita, ili nijipange upya na hilo ni kawaida kwenye soka, naamini dirisha litakapofunguliwa nitakuwa na uhuru wa kipi nikifanye. Japo Pamba imepanda msimu huu, lakini imesajili wachezaji wazuri, naamini tutafanya vizuri na nipo tayari kuipambania timu," alisema Mpole.

Mpole ambaye msimu wa 2021/22 alichukua kiatu cha Mfungaji Bora kwa mabao 17, alisema anajipanga kuhakikisha anafanya kitu kitakachomtambulisha kurejea kwake Ligi Kuu.

"Najua Ligi Kuu ina ushindani, nimejipanga kuhakikisha nafanya vitu vikubwa msimu ujao kwa kushirikiana na wenzangu ambao nipo nao kikosini," alisema aliyewahi kutamba na Real Nakonde ya Zambia, Mbeya City na Geita Gold.

Chanzo: Mwanaspoti