By Charles AbelMore by this Author Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limetupilia mbali malalamiko ya Simba kwa Al Merrikh ikidai iliwatumia wachezaji wawili waliofungiwa katika mchezo uliozikutanisha timu hizo jijini Khartoum, Sudan, Machi 6 mwaka huu.
Mara baada ya mchezo huo wa raundi ya tatu ya hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika uliomalizika kwa sare ya bila kufungana, uongozi wa Simba uliwaandikia Caf kuomba ufafanuzi wa kutumika kwa wachezaji Khamis Bakhit na Ramadan Agab ambao walikuwa wamefungiwa na Chama cha Mpira wa Miguu Sudan (SFA) kwa kosa la kusaini klabu mbili tofauti.
Hata hivyo licha ya Caf kutotangaza uamuzi wa malalamiko hayo, Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez amesema kuwa Caf imethibitisha kuwa wachezaji hao walikuwa halali kutumika na Al Merrikh kwa vile walikuwa wamefungiwa kushiriki mashindano ya ndani tu.
"Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (Caf) limetufafanulia kwamba wachezaji hao walifungiwa kucheza mashindano ya ndani hivyo wanaruhusiwa kucheza mechi yetu," alisema Barbara katika mahojiano yake na mtandao wa FilGoal wa Misri.
Kudhihirisha kuwa maombi hayo ya Simba kuhitaji ufafanuzi Caf yamekwama, Agab na Bakhit ni miongoni mwa wachezaji waliomo katika msafara wa timu hiyo uliotua nchini jana ukitokea Sudan tayari kwa mchezo baina ya timu hizo utakaochezwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa kesho Jumanne.
Ikiwa Simba wangefanikiwa katika rufaa hiyo, Al Merrikh wangeondolewa mashindanoni kwani wangekuwa wamekauka kanuni ya saba ya mashindano ya klabu barani Afrika.