Kocha Mkuu wa Simba SC, Roberto Oliviera 'Robertinho' ameweka wazi kuwa, pengo la kiungo wake mkabaji Sadio Kanoute litazibwa vizuri kesho na anaamini atakwenda kuibuka na ushindi katika mchezo wake dhidi ya Raja Casablanca.
Robertinho ameyasema hayo leo Februari 17, 2023 kwenye mkutano wa wanahabari kueleza maandalizi dhidi ya wapinzani wake hao mechi itakayopigwa katika Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.
"Nilipokuwa Dubai (kambini) niliandaa wachezaji wawili wawili katika kila nafasi na tunapouzungumzia mchezo wa kesho, ningependa kuongelea zaidi kwa kikosi kizima badala ya mchezaji mmoja mmoja. Tutamkosa Kanoute lakini yupo mchezaji mwingine atakayecheza nafasi hiyo," alisema Robertinho.
Simba anatupa karata yake ya pili ya mchezo wa Klabu Bingwa ikiwa ni hatua ya Makundi baada ya kupoteza kwa goli 1-0 dhidi ya Horoya mchezo walioanzia ugenini.