PSG wanakwenda kukipiga na mabingwa mara 13 wa Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya, timu ya Real Madrid kutoka Hispania hatua ya 16 bora.
Madrid wataanzia ugenini kisha watamalizia nyumbani katika harakati za kutafuta nafasi ya kuendelea kuweka ufalme Barani Ulaya.
Ndani ya PSG kwa sasa kuna wachezaji ambao washashinda Ubingwa wa Ulaya wakiwa na Real Madrid, yupo golikipa Keylor Navas ambae anasimama katika lango la PSG lakini yuko pia beki kisiki Sergio Ramos.
Ramos aliachana na Madrid katika dirisha lililopita baada ya kudumu klabuni hapo kwa miaka 16, sababu kubwa ikiwa ni kutaka apewe mkataba wa muda mrefu kuliko klabu ilivyotaka kumpa wa mwaka mmoja.
Akaondoka huru na kujiunga na Matajiri wa Ufaransa PSG, licha kuwa tangu atue klabuni hapo amekuwa akisumbuliwa na majeraha na amecheza mchezo mmoja tu katika ushindi wa magoli 3-1 dhidi ya St. Etienne, Novemba 28.
Sasa Ramos anarudi Santiago Bernabeu akiwa na PSG kusaka nafasi ya kwenda hatua ya Robo fainali na ameshaapa kuwa anakwenda kufa katika mchezo huo akiipigania PSG kupata ushindi.
"Kama ningekua na nafasi nisingechagua kucheza na Real Madrid, lakini kwa kuwa ndio imeshatokea nitapambana mpaka kufa" amesema Ramos akikiambia kituo cha Bein Sports
Michezo ya hatua ya 16 bora itapigwa Februari 15,16 kisha 22 na 23 huku ile ya marudiano ikipangwa kupigwa Machi 8,9 na 15, 16 mwakani.