Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Rais Samia azishushia neema Simba, Yanga

Rais Samia Akemea Rais Samia azishushia neema Simba, Yanga

Fri, 23 Aug 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Rais Samia Suluhu Hassan, amesema amefanya mazungumzo na wadau na wawekezaji wakubwa hapa nchini kwa ajili ya kuzidhamini klabu za Simba na Yanga ili ziendelee kufanya vizuri.

Akizungumza jana kwenye uwekaji wa jiwe la msingi kwenye ujenzi wa kituo cha michezo na ufundishaji cha Suluhu Academ, Kizimkazi, Zanzibar, Rais Samia, alisema amekuwa akizifuatilia timu hizo na siku zote yopo katikati na anafurahi pale zinapofanya vizuri.

"Najua wadhamini au washika vilabu hivi wanafanya jitihada kubwa sana, lakini pamoja nao nimeongea na wadau, wawekezaji wetu wakubwa hapa, mmoja nimempa Yanga, mmoja nimempa Simba awasaidie," alisema Rais Samia.

Aidha, alisema suala hilo litakapokamilika vilabu hivyo vitapewa taarifa na kuitwa kwa mazungumzo na hatua nyingine.

Katika hatua nyingine, Rais Samia, amesema kuwepo kwa viwanja vya kisasa vikiwemo vya soka kwa kiasi kikubwa kutaiwezesha Tanzania kuwepo katika ramani ya kimataifa na kuruhusu michezo mingi ya kimataifa kufanyika hapa nchini.

Alisema kuwepo kwa viwanja hivyo ni fursa ambayo itaiwezesha Tanzania kuandaa mashindano mbali mbali makubwa ya kimataifa zikiwemo fainali za Afrika, AFCON ambapo Tanzania inatarajia kuwa mwenyeji wa mwanza wa fainali za mwaka 2027 pamoja na nchi za Kenya na Uganda.

Aidha aliagiza kuendelea na kasi ya ujenzi wa viwanja ili vikamilike kwa wakati kwa ajili ya fainali hizo vikiwemo viwanja vinavyojengwa Arusha, Dodoma pamoja na Dar-es-Salaam.

Akizungumzia ujenzi wa kituo cha michezo Kizimkazi, aliwataka vijana kuchangamkia fursa za kuwepo kwa kituo hicho ambacho walengwa wake wakubwa ni kundi la vijana pamoja na watoto katika kukuza na kuibua vipaji vya michezo.

Alisema Vijana wanahitaji kuandaliwa mapema katika masuala mbali mbali ya msingi ikiwemo michezo hatua ambayo itawawezesha kuibuliwa kwa vipaji vyao na baadaye kuwa nyota wa michezo mbali mbali na kufikia kiwango cha kujiajiri.

''Akademi hii walengwa wake wakubwa ni kundi la vijana na watoto ambao vipaji vyao vitaibuliwa na kuweza kuvitumia katika maeneo mbali mbali na kuweza kujiajiri katika michezo''alisema..

Rais Samia, alisema wananchi wa Kizimkazi na Zanzibar kwa ujumla sasa wapo tayari kwa ajili ya ujenzi wa Akademi hiyo ya michezo ambapo wamechangia jumla ya Shilingi Bilioni mbili mradi huo ukamilike mwaka 2025 kama ilivyopangwa.

''Abebwaye hujikaza sisi wananchi wa Kizimkazi wilaya ya Kusini katika kuonesha utayari wetu wa ujenzi wa kituo cha michezo cha Suluhu Akademi tunachangia Shilingi bilioni mbili ili kuongeza ari kwa kushirikiana na wafadhili wetu'', alisema Rais Samia.

Akizungumza kwa upande wake, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, alisema Rais Samia amekuwa mdau mkubwa wa michezo mbali mbali kwa kuongeza hamasa kwa vilabu vya soka ikiwemo Simba na Yanga kuona vinapata ushindi mkubwa katika mashindano ya kimataifa.

Aidha alizitaja juhudi zinazochukuliwa na Rais Samia katika michezo ni pamoja na kuona ujenzi wa viwanja vya kisasa unafanyika nchini, hatua ambayo ni sehemu ya kuitangaza nchi katika ushindani wa soka na michezo mingine.

Aidha, mfadhili mnkuu wa mradi wa ujenzi wa kituo cha michezo chja Suluhu, benki ya CRDB kupitia Mkurugenzi Mtendaji wake, Abdulamajid Nsekela, alisema maandalizi ya ujenzi wa kiwanja cha kisasa cha Suluhu Akademi yameanza huku ujenzi huo ukitoa ajira kwa makundi mbali mbali ya wananchi wa kijiji cha Kizimkazi.

Nsekela alisema kituo hicho kikikamilika kitakuwa na uwezo wa kuchukua vijana 170 na kuwapatia mafunzo na kuwaandaa katika maeneo mbali mbali ya michezo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live