Kesho Jumanne Oktoba 25 katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya itashuhudiwa Dabi ya Mashemeji wakati Tanzania Prisons ikiikaribisha Polisi Tanzania katika mwendelezo wa Ligi Kuu Bara.
Kaimu kocha mkuu wa Polisi Tanzania, John Tamba amesema amekuwa akitumia muda mwingi kuongea na wachezaji ili kuwatia nguvu na kusahau mwanzo mbaya wa ligi walioanza nao.
"Tutajitahidi kupambana zaidi maana sio mchezo mwepesi kwetu hasa kwa kuangalia wapinzani wetu wanapokuwa kwenye uwanja wao wa nyumbani," anasema Tamba.
Mchezo huo utakuwa wa pili kwa Tamba kuiongoza Polisi Tanzania tangu kuondoka kwa Joslin Sharif na msaidizi wake, Agustino Damian kutokana na matokeo mabovu.
Kocha msaidizi wa Tanzania Prisons, Shaaban Kazumba amesema sare katika michezo miwili iliyopita (Ihefu na Mtibwa) imewafanya kuangalia wapi wanapojikwaa ili kesho wapate matokeo mazuri.
"Kila mchezaji anayonguvu ya kuhakikisha anafanya jukumu lake ipasavyo ili kuhakikisha tunapata alama tatu nyumbani," anasema Kazumba.
Nahodha wa Prisons, Benjamin Asukile amesema Polisi wamekuja Mbeya na kuanza kupata matokeo hivyo bado wanamatumaini kesho kuendelea kupata matokeo mazuri lakini nao wamejipanga.
"Tunajua kuzicheza dabi za majeshi, tunawaheshimu Polisi Tanzania maana wamekuwa tofauti na michezo iliyopita hivyo wanachokihitaji wao ndicho nasi tunachokihitaji," anasema Asukile.
Hata hivyo nahodha wa Polisi Tanzania, Tariq Simba amesema siku zote timu hizo zinapokutana unakuwa mchezo wa nguvu ndio maana hata mwamuzi anakuwa na kazi ya ziada.
"Tulikuwa tunapata matokeo mabaya na hicho ndio tulikuwa tunaumiza kichwa lakini haitawezekana kushuka daraja sababu ni hali ya mpito tu tunapitia," anasema Simba
Mchezo huo utachezwa saa 8:00 mchana katika uwanja wa sokoine jijini Mbeya badala ya saa 10:00 jioni kama ilivyofahamika hapo mwanzo.