Kocha Mkuu wa Singida Big Stars, Hans Pluijm amesema kuhusu ubingwa msimu huu atauongopea umma, lakini suala la kumaliza ndani ya Nne Bora lipo mikononi mwao kama watakomaa na mechi zilizosalia za msimu huu wa Ligi Kuu Bara.
Pluijm alisema duru la pili siku zote huwa ni ngumu kutokana na kila timu kuhitaji matokeo mazuri, hivyo kwao imebaki kupambana ili kumaliza nafasi nne za juu.
“Tunahitaji matokeo mazuri kwenye raundi ya hii ya pili na hili lipo kwenye wakati huu, ndio maana nasema hatma ya kumaliza nafasi nne za juu ni sisi wenyewe kupambana,” alisema Pluijm na kufichua kila mchezo katika ligi kwa sasa ni kama fainali na lengo ni kupata matokeo mazuri.
“Nimeshazungumza na wachezaji na kuwaambia tunatakiwa tucheze kwa kiwango cha hali ya juu kwa mechi zilizosalia na tutumie kila nafasi ambayo tunaipata kwenye mchezo na nafasi ipo mikononi kwetu,” alisema Pluijm.
Timu hiyo imepanda Ligi Kuu msimu huu kutoka Championship ilipotumia jina la DTB na inaundwa na wachezaji wakali kutoka ndani na nje ya nchi akiwamo kinara wao wa mabao Gomes Bruno anayetoka Brazil mwenye mabao tisa na staa wa zamani wa Simba, Meddie Kagere aliyefunga matano.