Watu sita wamekamatwa baada ya ofisi za Shirikisho la soka la Hispania pamoja na nyumba ya Rais wa zamani wa shirikisho hilo Luis Rubiales kuvamiwa na maafisa wa upelelezi kama sehemu ya uchunguzi.
Uchunguzi huo unahusu utakatishaji fedha na rushwa katika kashfa ya kuhamishwa kwa mashindano ya Super Cup ya Hispania kwenda Saudi Arabia.
Hadi sasa nyumba 11 zimepekuliwa juu ya kashfa hiyo inayokadiriwa kuwa na thamani ya pauni milioni 30.
Mamlaka nchini Hispania zimethibitisha kuwa Rubiales ni mmoja kati ya watu wengine watano ambao wameanza rasmi kuchunguzwa.
Maafisa hao hawakufanikiwa kumkuta Rubiales kwani taarifa zinaeleza kuwa yupo nje ya nchi.
Ofisi ya waendesha mashtaka wa Serikali ya Hispania imesema kuwa polisi wakishirikiana na wapelelezi wa Europol walikuwa wakitafuta nyaraka fulani.