JUMAPILI ya wiki hii Taifa Stars inacheza na Sudan mechi ya kuwania kufuzu fainali za AFCON, 2020 kiungo wa timu hiyo Erasto Nyoni amesema anaamini watawatoa kifua mbele Watanzania.
Nyoni ni kati ya wachezaji wazoefu ndani ya kikosi cha Stars, amesema mechi yao na Sudan si nyepesi, lakini wanajipanga kuhakikisha wanashinda nyumbani kabla ya kwenda kurudiana ugenini.
Amesema mazoezi wanayoyafanya chini ya makocha wao Etienne Ndayiragijje anasaidiana na Juma Mgunda pamoja na Seleman Matola anaamini yatawapa ushindi siku ya Jumapili.
"Tunajua mechi si rahisi ndio maana tunafanya mazoezi ya nguvu ya kutuweka fiti ili kuhakikisha wapinzani wetu hawafurukuti mbele yetu"
"Kwanza tujihakikishie ushindi nyumbani ndipo tutakapoanza kuwaza ya ugenini yatakuaje, tupo vizuri na dhamira yetu ni kushinda mechi hiyo"
"Jambo la mwisho niwaombe mashabiki wajitokeza kuiunga mkono timu yao, uwingi wao siku ya Jumapili ndio silaha yetu na kujiamini kwetu kwamba hatupo pekee yetu"amesema.
Pia Soma
- Arsenal, Man U waibeba England
- Azam FC yapewa mbinu za kuwafunga Triangle FC
- Maguli: Kwa Zesco, Yanga wawe makini mashambulizi ya pembeni
Kwa upande wa kocha Ndayiragije amesema amefanikiwa kuona mechi mbili za wapinzani wao hivyo anawafanyishaa mazoezi wachezaji kutokana na kile anachotarajia kwenda kukifanya siku ya Jumapili.
"Nimeona mechi mbili za Sudan kwa sehemu ninajua wanacheza mpira wa aina gani ingawa haitoshi kuishia hapo ninahitaji kwenda mbele zaidi kuhakikisha tunapata ushindi"amesema.