KIUNGO mshambuliaji wa Yanga, Haruna Niyonzima amesema wataingia kwa tahadhari kubwa katika mchezo ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Simba Mei 8 katika Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Yanga itaingia katika mchezo huo ikiwa imejikusanyia pointi 57, nne nyuma ya kinara Simba ambayo ipo kileleni ikiwa na pointi 61, huku ikiwa na michezo miwili mkononi.
Akizungumza na HabariLEO, Niyonzima alisema mchezo huo ni muhimu kwani wanahitaji matokeo zaidi ya wapinzani wao ili kurudi katika mbio za kulisaka taji la Ligi Kuu Tanzania Bara.
“Mchezo wetu dhidi ya Simba mara nyingi huwa mgumu sana, lakini soka lina matokeo matatu ambayo ni kushinda, kushindwa na kutoka sare, mwalimu ametueleza nini anataka wachezaji wote tunajua kwamba utakuwa mchezo mgumu,” alisema.
Niyonzima alisema mbinu walizopewa na Kocha wao Mkuu, Nassredine Nabi ambaye amekuwa akiwasisitiza kuongeza umakini kuhakikisha wanaondoka na pointi tatu katika kila mchezo ili kuongeza presha kwa Simba waliopo kileleni.
Alisema wao wanaamini bado wanaweza kutwaa taji hilo hivyo watapambana hadi dakika za mwisho.