KIUNGO wa Yanga, Haruna Niyonzima amesema kuwa licha ya ugumu wa raundi ya pili hawatakubali kurudia makosa, bali watahakikisha wanapambana kutwaa taji la Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.
Niyonzima aliyerejea kambini Yanga mwishoni mwa wiki iliyopita akitoka kwenye timu yake ya Taifa ya Rwanda, alisema wamekuwa wakiteleza lakini hali hiyo haitajitokeza tena hadi mwishi wa msimu.
Akizungumza na gazeti hili jana, Niyonzima alisema kwa jinsi walivyojipanga mwaka huu ni wakati wa kumaliza ufalme wa watani wao Simba ambao wametwaa taji la Ligu Kuu mara tatu mfululizo.
“Tuna uzoefu mkubwa na Ligi Kuu Tanzania Bara, mzunguko wa pili umekuwa na hesabu sana na sisi tumejipanga kuhakikisha tunamaliza michezo tukiwa kileleni na kushinda taji,” alisema Niyonzima.
Alisema mzunguko wa pili wa ligi ni mgumu kwani umegawanyika katika sehemu mbili, timu zinazopambana kutwaa ubingwa na zile zinazo pambana kutoshuka daraja hivyo kunaongeza ugumu katika mbio za kulisaka taji.
Pia alisema kitendo cha timu yao kuwa tena chini ya kocha Juma Mwambusi mwenye uzoefu wa Ligi Kuu Tanzania Bara ana amini wanaenda kuwa mabingwa kama walivyofanya akiwa chini ya makocha Hans Pluijm na George Lwandamina.