Msemaji wa Yanga, Haji Manara amemtwika mzigo mzito mshambuliaji mzawa, Ditram Nchimbi "Duma" kwa kumtaka afunge mabao mengi kwa msimu mpya wa 2021/22.
Manara ambae anasifika kwa kuwa[pa motisha wachezaji, amesema kuwa uwezo ambao anao Nchimbi ni mkubwa jambo ambalo anatakiwa kulifanya ni kushirikiana na wachezaji wenzake katika kufunga mabao na kuipa timu hiyo ubingwa wa 28 ndani ya Ligi Kuu Bara.
“Nchimbi ni mshambuliaji mzuri unaweza kumfananisha na Buffalo, (nyati) hivyo kwa msimu ujao kazi yake itakuwa ni kufunga mabao tu, Wananchi wanataka mabao ”.
Huo utakuwa ni mzigo mzito kwa Nchimbi kwa kuwa msimu wa 2020/21 katika jumla ya mechi 25 akitumia dakika 973 alifunga bao moja na kutoa pasi tatu za mabao.
Kinara wa utupiaji alikuwa ni Yacouba Songne ambaye alifunga jumla ya mabao nane ndani ya Ligi Kuu Bara na alitoa pasi sita za mabao.
Nchimbi ni mmoja wa Washambuliaji wazawa ambao wanakumbana na changamoto ya kupata nafasi kutokana na kusajiliwa kwa wachezaji wa kigeni katika eneo la mbele.