Mwandishi Wetu, Mwananchi
[email protected]
Dar es Salaam. Kelvin John ameendelea kuibeba timu ya Taifa ya vijana chini ya miaka 20, ‘Ngorongoro Heroes’ katika mashindano ya Kombe la Chalenji nchini Uganda.
Kelvin jana alifunga bao moja katika ushindi wa mabao 2-1 iliyopata Ngorongoro dhidi ya Sudan katika mchezo wa nusu fainali.
Matokeo hayo yamekuja zikiwa zimebaki siku chache kabla ya Taifa Stars kuivaa Sudan katika mchezo wa marudiano wa Fainali za Kombe la Mataifa Afrika Kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani (Chan)
Mshambuliaji huyo anaongoza kwa kufunga mabao saba katika mashindano hayo yaliyoshirikisha timu 11 na Andrew Simchimba amefunga sita.
Pia Soma
- Yanga, Polisi vitani
- Kipigo cha Spurs chaweka rekodi
- Mrembo Gigi avaana na aliyevamia jukwaa la Fashion Show
Timu hiyo iliyopangwa Kundi B ilianza hatua ya makundi kwa kuifunga Ethiopia mabao 4-0, ilitoka sare 2-2 na Kenya kabla ya kuilaza Zanzibar 5-0 na kutinga robo fainali.
Katika robo fainali Ngorongoro iliichapa Uganda mabao 4-2 kabla ya jana kuicharaza Sudan.
Kocha wa Ngorongoro Zuberi Katwila alisema wachezaji wake wamefuata maelekezo yake na matarajio yake ni kutwaa ubingwa wa mashindano hayo.
Alisema kila mchezaji alikwenda uwanjani akiwa amepewa majukumu ya kufanya baada ya kuishuhudia Sudan.
“Nawapongeza wachezaji wangu kila mechi wanapambana na kufuata maelekezo yangu, mechi na Sudan ilikuwa ngumu lakini tumefuzu fainali,” alisema Katwila.
Kocha huyo wa Mtibwa Sugar alisema anatarajia mchezo wa fainali Oktoba 5 utakuwa mgumu na mkakati wake ni kufanya vyema.