KOCHA wa timu ya Soka ya taifa, Taifa Stars, Etienne Ndayiragije amesema mipango aliyonayo ni kuwapa mbinu mpya wachezaji wake zinatakazo wafanya kuibuka na ushindi kwenye mchezo dhidi ya Guinea utakaochezwa kesho.
Stars iliyopangwa Kundi D katika Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa nyumbani (Chan) wanahitaji ushindi kwenye mchezo huo ili kujihakikishia kutinga hatua ya robo fainali.
Mchezo huo unatarajiwa kuwa mgumu kwa Stars kwani wanaenda kukutana na Guinea ambao ni vinara wa kundi hilo wakiwa na pointi nne sawa na Zambia wanaoshika nafasi ya pili wakitofautiana kwa mabao ya kufunga, Stars wakikalia nafasi ya tatu na pointi tatu huku Namibia wakishika mkia.
Akizungumza kutoka Cameroon ambako michuano hiyo inachezwa, Ndayiragije alisema anajiamini na wachezaji alionao na wamejifunza mengi, hivyo mbinu mpya zinaweza kuwavusha dhidi ya Guinea.
“Mchezo utakuwa mgumu, ushindi wa mchezo uliopita wa bao 1-0 dhidi ya Namibia ni morali kwa wachezaji wangu,nimewaangalia wapinzani wetu utakuwa mchezo mgumu lakini hata sisi tunayo nafasi ,”alisema Ndayiragije.
Mchezo dhidi ya Guinea utakuwa wa mwisho wa kuamua timu mbili zitakazo songa hatua inayofuata na zingine mbili kuaga michuano hiyo kujipanga upya kwa msimu mwingine ujao.
Katika hali isiyotarajiwa beki mkongwe Erasto Nyoni aliyechelewa kujiunga na kikosi hicho Cameroon kwa matatizo ya kifamilia alirejea nchini jana asubuhi huku akigoma kuzungumza na wanahabari kueleza sababu iliyomfanya arudi mapema wakati kikosi hicho kikiwa na kibarua dhidi ya Guinea kesho.
Nyoni anayeicheza klabu ya Simba, ndiye mchezaji pekee aliyeshiriki fainali za kwanza za michuano hiyo zilizochezwa Ivory Coast mwaka 2009 na Tanzania kuishia hatua ya makundi.