Kocha msadizi wa Yanga, Cedric Kaze amesema mchezo wao dhidi ya Namungo utakuwa mgumu kutokana na ubora wa timu zote mbili pindi wanapokutana.
Kwenye mechi sita za mwisho ambazo wamekutana Yanga imeshinda mchezo mmoja tu na mechi zingine kuisha kwa sare.
Mchezo ambao Yanga imeshinda ni ambao walikuwa nyumbani kwenye uwanja wa Mkapa na mechi tatu zote walizotoka sare ni wakiwa ugenini.
Akiungumza na Waandishi wa Habari jioni hii, Kaze amesema anajua kabisa wapinzani wake wana benchi la ufundi bora ambalo linaleta ushindani kwenye Ligi.
"Wana wachezaji na benchi la ufundi lenye kuijua ligi kwahiyo mchezo wa kesho utakua mgumu, tunatakiwa kutumia kila nafasi ambayo itapatikana," amesema Kaze na kuongeza;
"Tunaingia kwenye mchezo huu kwa tahadhari kubwa na hatutoangalia uwiano wa kwenye msimamo wa ligi."
Kaze amesema kwenye mchezo huo wanatakiwa kuhakikisha wanapata pointi tatu lakini wanatakiwa kujilinda na kushambulia.
Upande wa mchezaji wa timu hiyo, Zawadi Mauya amesema mchezo huo utakuwa mzuri kutokana na namna ambavyo wote wamejiandaa.
"Tunajua hakùna mchezo rahisi kwenye ligi, sisi kama wachezaji huwa tunaongea kabla na baada ya mchezo kuona wapi tumefanya vizuri na wapi tumekosea, kwahiyo tutarajie kuwa na mchezo mzuri," amesema Mauya.
REKODI ZAO
15/03/2020 Namungo 1-1 Yanga
24/6/2020 Yanga 2-2 Namungo
22/11/2020 Yanga 1-1 Namungo
15/5/2021 Namungo 0-0 Yanga
20/11/2021 Namungo 1-1 Yanga
23/04/2022 Yanga 2-1 Namungo