Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Mohammed Nabi amesema anajivunia wachezaji wa kikosi chake kutokana na upambanaji wao waliouonyesha kwenye mchezo dhidi ya Dodoma Jiji FC.
Mchezo huo uliopigwa kwenye dimba la CCM Liti mkoani Singida ulimalizika kwa Wananchi kubeba alama tatu baada ya ushindi wa mabao 2-0.
Nabi amesema walikutana na timu ngumu sana lakini wachezaji wake walijituma mno kuhakikisha wanaondoka na ushindi.
“Dodoma ni timu ngumu inayocheza soka la nguvu sana. Walitupa wakati mgumu na wachezaji wangu walikuwa bado na mchoko wa safari.
“Lakini unaweza kuona namna vijana walivyojitoa na kupambana kuhakikisha tunashinda mchezo huu. Najivunia sana wachezaji wangu na huu ni ushindi wa zawadi kwa mashabiki wetu,” alisema Nabi.