Wakati Yanga SC , ikijiandaa na mchezo wa kesho dhidi ya Kagera Sugar, kocha wa timu hiyo, Nasreddine Nabi amelalamikia ugumu wa ratiba ya ligi na kwamba wachezaji wake hawajafanya mazoezi tangu Jumatano.
"Tumefika Mwanza jana (juzi) usiku na tuna siku moja tu ya mazoezi. Hii sio rafiki kwa afya ya mwili wa wachezaji," amesema Nabi
Nabi amesema lengo sio kulalamika ila viongozi wa mpira wanapaswa kuliangalia jambo hilo kwa jicho la tatu.
Ameeleza kuwa kiakili wachezaji wako vizuri kinachosubiriwa ni ripoti ya madaktari kujua utimamu wa miili yao kabla ya kuanza mazoezi jana jioni.
"Kucheza Yanga ni kujitoa na huu ni wakati ambao Wachezaji wetu wanatakiwa kujitoa sana kwa ajili ya timu yao. Wamekosa muda wa kupumzika lakini wanajua wamekuja Mwanza kupambana," amesema Nabi.
Aidha kocha msaidizi, Cedric Kaze amesema baada ya Aziz Ki kufungiwa mechi tatu ataruhusiwa kurudi kwao kujiunga na timu yake ya Taifa.