HABARI njema kwa mashabiki wa Yanga ni kwamba staa wao, Saido Ntibazonkiza aliyekuwa anasumbuliwa na nyama za paja ameanza kukiwasha mdogomdogo huko Burundi kwenye timu ya Taifa.
Saido ambaye alikuwa majeruhi tangu mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara uanze, juzi jioni aliibukia kwenye mazoezi ya timu ya Taifa ya Burundi na jana pia alipasha asubuhi na mchana akaenda kufanyiwa vipimo kwa mujibu wa kiongozi wa Shirikisho la Soka la Burundi. Hiyo inamaanisha kwamba Saido kama ataendelea kuimarika atakuwemo kwenye kikosi cha Yanga kitakachocheza FA dhidi ya Prisons siku ya Jumapili ya Pasaka.
“Ameanza mazoezi mepesi tunategemea Ijumaa ataanza kuchezea mpira na wenzie lakini tunamfanyia vipimo tena kujiridhisha kwamba yuko sawa, ila tunaamini ikichelewa sana Jumatatu atakuwa uwanjani,” alisema kiongozi huyo huku akihofia kwamba endapo wakimtumia akiumia zaidi wanaweza kumharibia kibarua chake Yanga. Burundi inajiandaa na mechi ya kufuzu Afcon dhidi ya Afrika ya Kati Ijumaa ijayo.
MZUKA MAZOEZINI
Mastaa wa Yanga licha ya kwamba wanalalamika kimoyomoyo kwamba matizi ya Kocha Juma Mwambusi si mchezo, lakini wanayakubali kwamba yanawajenga kwenye pumzi.
Farouk Shikhalo ambaye ni kipa Mkenya, alisema kama kuna mashabiki wanamchukulia poa Mwambusi basi wanakosea kwani katika siku mbili tu amewachangamsha na kuwarudisha kwenye mzuka wa kazi.