Tuzo ya Mchezaji Bora ya NIC Insurance kwa mwezi Januari ndani ya Yanga SC, imechukuliwa na Clement Mzize baada ya kuwashinda Gift Fred na Wilson Chigombo ambao aliingia nao fainali.
Mzize ameshinda tuzo hiyo inayotolewa na Shirika la Bima la Taifa (NIC) baada ya kupata kura kwa asilimia 55.
Wakati Mzize akiwa namba moja, Fred alipata kura asilimia 30, huku Chigombo akiambulia asilimia 15.
Mashabiki na wanachama wa Yanga SC, ndio wamekuwa na jukumu la kumchagua mshindi wa tuzo hiyo kila mwezi kutokana na kupiga kura kupitia Application ya Yanga SC.
Tuzo hizo zilianza kutolewa mwezi Oktoba 2023 chini ya udhamini wa NIC kwa kushirikiana na Klabu ya Yanga, ambapo mshindi wa kwanza alikuwa Stephane Aziz Ki, akafuatia Pacome Zouzoua aliyeshinda mwezi Novemba, huku Djigui Diarra akiwa mshindi mwezi Desemba.
Mzize baada ya kuibuka mshindi wa Tuzo ya NIC Insurance Mwezi Januari, anatarajiwa kukabidhiwa kiasi cha shilingi milioni nne (4,000,000).