Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mziki wa Ouma washtua Coastal

Ouma Coasta.jpeg Mziki wa Ouma washtua Coastal

Wed, 5 Jun 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Kuongoza timu hadi kufanikiwa katika nchi ya kigeni si kazi rahisi kwa kocha yeyote yule.

Ndio maana wakati kocha Mkenya David Ouma alipokubali ofa ya kuwa kocha mkuu wa Coastal Union ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Novemba mwaka jana, alikuwa na kibarua kikubwa cha kuondoa timu hiyo katika hatari ya kushushwa daraja.

Miezi sita tu baada ya kujiunga na timu hiyo, Ouma ana furaha kuiwezesha Coastal Union kumaliza katika nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi na kujikatia tiketi ya kucheza Kombe la Shirikisho Afrika (CAFCC) baada ya miaka 36.

Coastal Union imeshika nafasi ya nne ikiwa na pointi 43, ikiwa nyuma ya vinara, Yanga kwa pointi 37.

Azam FC na Simba SC zimeshika nafasi ya pili na tatu kwenye jedwali zikiwa na pointi 69 kila moja. Hata hivyo, Azam iliambulia nafasi ya pili kutokana na tofauti kubwa ya mabao.

Ouma, akiongea kipekee na Mwanaspoti alisema kuwa lengo lake lilikuwa kumaliza ndani ya nafasi nne bora.

"Kwa kuelewa utamaduni wa klabu na asili ya wachezaji, nilitambua hitaji la kuimarisha uchezaji wao na kustawisha furaha katika mchezo wao," alisema Ouma ambaye alichukua mikoba ya kocha wa DRC, Mwinyi Zahera.

"Morale ilikuwa chini sana nilipojiunga na timu hii. Nilileta uchangamfu kwa timu na timu ilikuwa inaelekea kushuka daraja. Hili si jambo rahisi kwa kocha yeyote mgeni kwenye timu. Wakati msimu ukiendelea, wachezaji walijikuta wakiwania ubingwa wa ligi," aliongeza Ouma.

Timu hiyo ilijikusanyia pointi 35 baada ya Ouma kuchukua nafasi hiyo, na kupata kupanda hadi nafasi ya nne kutoka nafasi ya 14. Walidumisha nafasi hiyo ya nne katika mechi za mwisho za mkondo wa kwanza na kuidumisha hadi mkondo wa pili.

Katika kampeni zao, Coastal Union ilishinda mechi 11, ikatoka sare mara 10, na kupoteza michezo tisa. Mechi ya kwanza ya timu hiyo chini ya uongozi wa Ouma ilizaa ushindi wa 1-0 dhidi ya Prisons Novemba mwaka jana.

Kufuatia mchezo huo mzuri, kipa Lameck Lawi aliitwa kwa majukumu ya timu ya taifa, Taifa Stars, kwa maandalizi ya mechi ya kufuzu Kombe la Dunia 2026 dhidi ya Zambia mwezi huu.

Kwa tuzo binafsi, kipa wa Coastal Union ya raia wa Congo, Ley Matampi ameingia kuwania tuzo ya kipa bora wa ligi wa msimu akiwa hajafungwa bao katika mechi 15 (clean sheets). Mlinda lango wa mabingwa mara tatu mfululizo, Yanga, raia wa Mali Djigui Diarra, ana clean sheets 14.

Beki wa Coastal Union, Daudi Semfuko, 18, alikuwa mchezaji mdogo zaidi kiumri kwenye ligi. Amefunga mabao manne msimu huu na pia yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuwania tuzo ya Mchezaji Mdogo zaidi wa Msimu.

"Nikitafakari safari hii, kwa kweli nimeridhishwa na ukuaji na uthabiti wa timu, uliowekwa na maadili ya kazi na uthubutu. Nashukuru pia uongozi wa Union ambao umenipa sapoti pamoja na mashabiki ambao wamesimama nasi tangu nichukue kazi hii," aliongezea Ouma.

Licha ya kutozingatiwa awali kuwa wagombea wa nne bora, Union imekaidi matarajio msimu huu.

Wengi walitabiri Singida Fountain, ambayo ilimaliza nafasi ya 11, ingetwaa ubingwa kwa sababu ya uwepo wa wachezaji nyota wa kigeni ambao ni Wakenya Joash Onyango (beki), Elvis Rupia (mshambuliaji) na Duke Abuya (kiungo).

Alijiunga na timu hiyo kutoka kwa Sofapaka inayoshiriki Ligi Kuu ya Wanaume ya Shirikisho la Soka nchini (FKF-PL) akiwa ameshikilia wadhifa wa Mkurugenzi wa Michezo hapo awali akiwa kocha mkuu msimu wa 2022/23 kabla ya Zedikiah Zico kuchukua wadhifa huo.

"Ninafurahi kwamba, kile nilichokifanya katika soka la Kenya kwa miaka mingi nililazimika kukifanya kwa majirani zetu. Katika mazingira mapya na watu wapya, nilijiunga na klabu kubwa zaidi barani Afrika baada ya kukataa ofa kutoka Ethiopia na Afrika Kusini," aliongeza Ouma.

Haya yalikuwa majukumu yake ya kwanza nje ya Kenya.

Kando na kufundisha timu za wanaume, Ouma alijizolea umaarufu mkubwa katika soka la wanawake nchini Kenya.

Aliongoza timu ya Taifa ya Wanawake ya Kenya, Harambee Starlets, kucheza kwa mara ya kwanza katika michuano ya Wanawake ya Mataifa ya Afrika (WAFCON) mnamo 2016.

Kwa bahati mbaya, Kenya haikuweza kufuzu kwa raundi inayofuata katika kundi gumu lililoshirikisha Ghana, Nigeria, na Mali, ambapo Kenya ilipoteza 3-1, 4-0, na 3-1 mtawalia.

Miaka mitatu baadaye, Ouma aliiongoza Starlets kunyakua ubingwa wa Cecafa kwa Wanawake mwaka 2019 kwa kuwalaza Twiga Stars ya Tanzania mabao 2-0 katika fainali iliyochezwa kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam, na kutwaa taji lao la kwanza.

Akawa kocha wa kwanza kuwahi kufikia hili katika soka la wanawake.

Mnamo Aprili 2021, baada ya Nick Mwendwa kuchukua wadhifa kama rais wa FKF nchini Kenya, akimrithi Sam Nyamweya, Ouma alitangaza kujiuzulu wadhifa wake wa ukufunzi katika timu ya taifa.

Lakini alijiunga tena na Sofapaka ya FKF-PL kama kocha msaidizi wa Ken Odhiambo siku tatu tu baadaye ya kuachana na Starlets.

Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, ligi za wanaume na wanawake nchini Tanzania zimepata umaarufu barani Afrika, hivyo kuwavutia wachezaji wengi wanaotaka kuhamia huko.

Licha ya ubora wa ligi ya Tanzania, ni Watanzania wachache tu kama mshambuliaji Mbwana Samatta ambaye kwa sasa anakipiga katika klabu ya PAOK FC ya Uturuki wamejitosa nje ya nchi kujitangaza kisoka.

Kulingana na kocha Patrick Odhiambo, mkufunzi wa zamani wa Biashara United ya Tanzania ambaye sasa anafundisha timu ya Kakamega Homeboys ya FKF-PL anasema, “Katika siku za hivi karibuni, wachezaji wa Tanzania sasa wameanza kuhamia katika ligi tofauti tofauti kote duniani. Inamaana kuwa, soka la Tanzania limeanza kukua kwa kiasi kikubwa. Ligi ya Tanzania sasa inajulikana hata nje ya Afrika," alisema Odhiambo.

Lakini kiuhalisia, umaarufu wa soka la Uingereza una umaarufu sana nchini Kenya ikilingwanishwa na soka la nyumbani.

"Mashabiki wa Tanzania, wadogo na wakubwa, wanadhihirisha hamasa kwa ligi yao, wakienda kushuhudia mechi kwa amani tofauti na vurugu za mashabiki mara nyingi zinazoshuhudiwa Kenya, zinazozuia familia kuja na watoto wao kutazama mechi," Odhiambo alisema.

Odhiambo pia alitambua mashabiki wa Tanzania kwa nidhamu yao kwenye michezo, kununua jezi zinazostahili na kutenganisha soka na siasa.

Pia alifanya kazi kama msaidizi wa Steven Polack kwa mabingwa watetezi wa FKF-PL, Gor Mahia musimu wa 2019/20. Pia, ni kocha wa zamani wa Western Stima, Agro Chemicals, Muhoroni Youth, Chemelil Sugar, na Sony Sugar, washindi wa ligi ya FKF-PL ya mwaka 2006.

Wachezaji wengi wa soka wa Kenya, wanaume na wanawake, wamehamia nchi Tanzania kutokana na ada nzuri za usajili, mikataba bora, mishahara mikubwa, na matibabu bora kwa ujumla yanayotolewa na klabu.

Bernard Mwalala, mshambuliaji wa zamani wa kimataifa wa Kenya na mchezaji wa zamani wa Yanga ambaye sasa anahudumu kama kocha mkuu wa KCB, klabu ya FKF-PL, anakiri kuwavutia wachezaji wa Ulaya kutafuta ushindani bora kwenye ligi ya Tanzania.

"Ligi ya Tanzania imeboreshwa sana katika miaka 15 iliyopita. Zamani karibu na mwaka 2006, tulipata Tsh600,000 kwa mwezi, lakini sasa wachezaji wanaweza kupata hadi Tsh milioni 10 ikiifanya kuwa moja ya ligi zenye umaarufu mkubwa katika Afrika Mashariki. Inaweka changamoto nzuri kwa Kenya; sisi pia tunaweza kujitahidi kufanya vizuri. Wachezaji wengi wa Tanzania hawachezi Ulaya kwa sababu wanahudumiwa vyema nyumbani," alisema Mwalala.

Utamu wa ligi ya Tanzania pia unaongezeka kutoka na debi ya Kariakoo kati ya Yanga na Simba, huku debi ya zamani ya Kenya ya Mashemeji kati ya Gor Mahia na AFC Leopards ikiendelea kupoteza ladha.

Kocha MKenya Francis Baraza ambaye kwa sasa ndiye kocha mkuu wa Dodoma Jiji alielezea kuwa, kuna tofauti kubwa kati ya mwabiki wa soka la Kenya na Tanzania.

"Watu Tanzania wanapenda mechi zao wenyewe. Kwa soka la Ulaya, mashabiki wanapotazama mpira katika maeneo ya migahawa, huwa wanapunguza sauti na kutazama video pekee huku wakisikiza muziki. Lakini kwa mechi za ligi za ndani, wanapenda kuwasikiza watangazaji wao wa nyumbani," alisema Baraza.

Michezo ni tasnia yenye thamani ya mabilioni ya dola. Biashara ya soka nchini Tanzania inazingatia zaidi shughuli za biashara.

Kocha wa zamani wa makipa wa Biashara United ya Tanzania, John Waw ambaye kwa sasa yuko Homeboyz anasema, mechi kuonyeshwa kwenye televisheni, kuuza jezi na bidhaa za timu, inachangia kuzikuza klabu.

Simba, Azam na Yanga wamefanikiwa katika jambo hili.

"Upatikanaji wa wadhamini, viwanja bora vya kuchezea, usimamizi mzuri pamoja na mishahara ya ushindani vimewasaidia wachezaji wa Tanzania kukua. Wachezaji wanapewa kila kitu na ndio maana kuna ushindani mkubwa Tanzania," alisema Waw.

Nsue amefungiwa kucheza soka la kimataifa kwa kipindi cha miezi sita na shirikisho la soka la Equatorial Guinea (Feguifut) limepigwa faini ya Pauni 131,000. Hukumu hiyo imetolewa kutokana na Nsue kuichezea timu ya vijana ya Hispania kwenye mechi za kimataifa kabla ya kuhamia kwenye kikosi cha timu ya wakubwa ya Equatorial Guinea bila ya kuruhusiwa na Fifa.

Mwaka 2013, Fifa iliambia Feguifut mchezaji huyo amepata tu uraia wa nchi hiyo, lakini tayari alicheza mechi yake ya kwanza ya kimataifa ya kimashindano. Baada ya Nsue kucheza mechi mbili kwenye timu ya Equatorial Guinea ilitambulika kwamba hapaswi kuendelea kuitumikia timu hiyo kwenye soka la kimataifa na hivyo, Equatorial Guinea kuvuliwa ushindi wa mechi hizo mbili za kufuzu Kombe la Dunia 2014 kwa kipigo cha 3-0.

Nsue aliichezea Hispania mechi 26 za kimataifa kuanzia kwenye timu za vijana chini ya umri wa miaka 16 hadi chini ya miaka 21, ambapo alishiriki kwenye michuano ya kuwania ubingwa wa Ulaya kwa timu za vijana chini ya miaka 21 mwaka 2011.

Fifa inafichua kwamba Guinea iliomba ruhusu kutoka kwenye chama cha soka Hispania, lakini haikuomba kupitia Fifa. Hadi sasa, staa huyo mwenye umri wa miaka 34, amecheza zaidi ya mechi 40 na kuifungia mabao 23 timu hiyo, ikiwamo mabao matano kwenye Afcon 2023 iliyofanyika Januari mwaka huu. Nsue, ambaye aliwahi kuzichezea Mallorca, Middlesbrough na Birmingham City, aliisaidia timu yake kuongoza Kundi A kwenye fainali hizo zilizofanyika Ivory Coast, kabla ya timu hiyo kukomea kwenye hatua ya 16 bora ilipochapwa na Guinea.

Nsue, ambaye anachezea klabu ya Daraja la Tatu Hispania, Intercity, anaweza kukata rufaa kupinga hukumu hiyo ya Fifa kwenye mahakama ya rufani ya michezo (Cas).

Chanzo: Mwanaspoti