Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mwenda apewa mbinu mbele ya Kapombe

Mwenda Pic Data Beki wa Simba, Israel Patrick Mwenda apewa mbinu

Wed, 8 Dec 2021 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

Beki wa kulia wa Simba, Israel Patrick Mwenda amepewa mbinu za kukaa kwenye ushindani wa namba mbele ya Shomari Kapombe ambaye amekuwa bandika bandua kikosi cha kwanza.

Kitendo cha kocha Pablo Franco, kumuanzisha mechi ya Kombe la Shirikisho Afrika (CAF) dhidi ya Red Arrows na Mwenda kuonyesha kiwango kikubwa, kimewaibua wadau kumpa ushauri.

Meneja wa Mbeya Kwanza, Emmanuel Gabriel alisema alichokionyesha Mwenda dhidi ya Red Arrows, Simba ikiibuka na ushindi wa mabao 3-0 mechi ya kwanza, Uwanja wa Mkapa, kinampa nguvu kocha kumpa nafasi mechi mbalimbali.

“Japokuwa Kapombe ana uzoefu mkubwa na michuano ya kimataifa kutokana na kucheza kwa muda mrefu, lakini Mwenda naye anapaswa kutazama kwa jicho kubwa kwa msaada ndani ya timu hiyo,”alisema Gabriel ana akaongeza kuwa;

“Kila mchezaji ana kitu chake, Mwenda alijitahidi kuonyesha uwezo wake licha ya kutokuwa mzoefu kwenye michuano hiyo, kocha akiendelea kumpa nafasi atakuwa beki mzuri zaidi,”alisema.

Kauli yake ilipigiliwa msumari na aliyekuwa beki wa timu hiyo, Amir Maftah aliyesema Mwenda ni kijana aliye na kitu kwenye mguu wake, endapo akipata nafasi ya kucheza anamuona mbali.

“Jambo analopaswa kuzingatia Mwenda, ajue anacheza na Kapombe anayejipambanua vyema kwenye majukumu yake, ajifunze na afanye bidii kwa mambo yanayotakiwa kwenye soka,”alisema.

Alisema hadi viongozi wa Simba walimsajili Mwenda kutoka KMC waliona kitu mguuni kwake anachopaswa kukipigania bila kujisahau na raha za mashabiki wake.

“Kinachowasahaurisha chipukizi wengi wakifika Simba na Yanga, hawajui kusajiliwa ni hatua moja na kuonyesha uwezo ni hatua ya pili kudumu na kiwango ni jambo lingine, lazima wajipambanue zaidi watafika mbali,” alisema.

Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz