Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga, Ali Kamwe ametozwa faini ya Sh1 milioni kwa kosa la kumkejeli na kumdhalilisha mwamuzi wa mechi ya Singida Big Stars dhidi ya Simba kupitia mtandao wa kijamii.
Maamuzi ya kumtoza faini Kamwe, yamewekwa wazi katika taarifa ya Bodi ya Ligi Kuu, iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo Alhamisi Oktoba 19, 2023 jijini Dar es Salaam.
"Baada ya kumalizika kwa mechi, Ali Kamwe aliweka chapisho katika ukurasa wake binafsi wa mtandao wa kijamii wa Instagram, ambalo lilikuwa na picha ya mwamuzi (Malogo)," imeeleza taarifa hiyo na kuongeza;
"Huku akiunganisha na wimbo wa msanii wa muziki kizazi kipya, Billnass uitwao Maokoto, hali iliyoleta tafsiri ya kumhusisha mwamuzi huyo na masuala ya fedha ama rushwa."