Kipa mpya wa Azam FC, Mohamed Mustafa amefichua kwamba miongoni mwa vyakula ambavyo anapenda kula tangu alipotua nchini akitokea kwao Sudan, ni pamoja na mihogo na kachumbari kwa pembeni iwe ya kukaanga au kupika.
Elewa kwamba Mustafa hata ukimpa mihogo ale mara mbili kwa siku, basi kwake freshi tu na zaidi utakuwa umeugusa moyo wake.
Mustafa ametua Azam FC kwa mkopo wa miezi sita akitokea Al-Merrikh ya Sudan ili kuziba pengo za Abdulai Iddrisu na Ali Ahamada ambao watakuwa nje ya uwanja kwa kipindi kirefu wakiuguza majeraha.
"Napenda sana mihogo. Nimekuwa nikitoka nje (ya kambi) ili kuhakikisha napata hicho chakula. Nimeona kwa Tanzania ni maarufu sana maeneo mengi hupikwa. Nimekuwa nikila mara mbili kwa siku," amesema.
Kisha akaongeza kuwa, "ujue hata nyumbani kwetu Sudan mihogo ipo, lakini imekuwa ikitengenezwa kwa aina tofauti na huku. Kule imekuwa ikipikwa kabisa na kuchanganywa na viungo vingine. Ni mitamu balaa."
Mustafa aliyezaliwa Februari 19, 1996 anatarajiwa kuanza kutumika kwenye michezo ya Ligi Kuu Bara kwa mara ya kwanza wikiendi hii wakati Simba itakapoikaribisha Azam kwenye mchezo wa kiporo ambao unatarajiwa kupigwa katika Uwanja wa CCM Kirumba huko jijini Mwanza.