Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Msolla: Tusimpe kocha presha

C159b03849f6bebadda6100967606e5f Msolla: Tusimpe kocha presha

Sat, 17 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MWENYEKITI wa Klabu ya Yanga, Dk Mshindo Msolla amewahimiza mashabiki na wapenzi wa klabu hiyo kuwa watulivu na kuepuka kumpa presha kocha wao mpya, Cedric Kaze atakapoanza majukumu yake.

Akizungumza jana Dar es Salaam wakati akisaini mkataba na kocha huyo sambamba na kumtambulisha, Dk Msolla alisema Kaze anahitaji nafasi ili afanye kazi yake vizuri.

Kaze ambaye ni raia wa Burundi, amesaini mkataba wa miaka miwili ila kuna kipengele cha kuongeza baadaye kama itahitajika na wakati wowote anatarajiwa kuanza majukumu yake mara atakapopata vibali vya kazi.

“Tumpunguzie presha mwalimu, tumpe nafasi afanye kazi yake, tusitake matokeo basi anaanza kesho, tumpe ushauri nina imani hata yeye anahitaji matokeo mazuri,” alisema Dk Msolla ambaye pia ana taaluma ya ukocha.

Dk Msolla alisema huyo ndiye mwalimu waliyemuhitaji kwa muda mrefu na hivyo, wamefurahi kumpata na kwamba anaamini ni chaguo sahihi kwao.

Alisema kocha huyo atafanya kazi na Kamati ya Ufundi na kwamba wao kama viongozi wapo tayari kumpa ushirikiano kwa asilimia 100 na wamepanga utaratibu ili kila wiki akutane na viongozi kujadiliana masuala mbalimbali kama yapo kwa ajili ya kuboresha.

Kwa upande wake, Kaze alishukuru viongozi, mashabiki kwa mapokezi mazuri na kuahidi kuendeleza yale mazuri yaliyoachwa na kocha aliyefungashiwa virago, Zlatko Krmpotic.

Alisema anasubiri kuanza kwa majukumu yake kwani watu wengi wanatamani kuona kama wataweza. “Nashukuru kwa sapoti niliyopata kutoka kwa timu, viongozi na mashabiki, hamuwezi kuamini watu wanapenda Yanga.

Nimepata ujumbe nyingi kutoka ulimwenguni, watu wako Marekani, Ulaya na sehemu mbalimbali, sitaki kuongea mengi nasubiri kuanza majukumu yangu,” alisema Kaze aliyetua nchini juzi usiku akitokea Canada.

Alisema kitu cha kwanza anachoweka mbele ni wachezaji kwani wao ndio watakaowapatia mashabiki furaha huku pia akisema anaijua ligi ya Tanzania na viwanja vyake, kwani hilo halitampa tabu kwa kuwa wanaweza kubadilika kulingana na wapi watakuwepo.

Pia alisema katika mfumo wake hapendi mchezo wa kupoteza muda, bali kumiliki mpira na kushambulia kwa kasi. Kwa upande wake, Mshauri wa Yanga, Senzo Mbatha aliwashukuru wadhamini wote wa klabu hiyo kwa kuendelea kuwaunga mkono huku akimuahidi kocha huyo ushirikiano wa kutosha ili kufanya kazi yake vizuri.

Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Patrick Simon alisema ataanza kushughulikia vibali vya kocha na kuomba mashabiki na wanachama kuwaunga mkono

Chanzo: habarileo.co.tz