Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Gerson Msigwa amesisitiza kuwa uwanja wa mpira wa miguu unaojengwa Jijini Arusha kwa ajili ya michuano ya AFCON 2027 utawanufaisha wananchi kiuchumi huku akiwataka vijana wa Jiji hilo wajiandae kunufaika na ajira zitakazotokana na ujenzi huo.
Katibu Mkuu, Gerson Msigwa ameyasema hayo alipotembelea eneo la ujenzi wa uwanja huo Kata ya Olmoti Jijini Arusha kukagua maendeleo ya ujenzi huo ambapo amesema Mkandarasi kwa sasa anaendelea na hatua za awali za ujenzi huo huku akisisitiza kuwa utakamilika kwa wakati ili utumike katika michuano ya AFCON 2027.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Suleiman Serera aliyeambatana na Katibu Mkuu Msigwa katika ziara hiyo ameeleza kuwa ujenzi wa uwanja huo una maana kubwa kwa Jiji la Arusha kwa kuwa umefungamanishwa na ukuaji wa sekta nyingine za kiuchumi ikiwemo Utalii kwa kuwa Arusha ni kitovu cha Utalii nchini Tanzania.