Kipa wa Yanga, Aboutwalib Mshery ameongeza mkataba wa miaka mitatu kuendelea kuitumikia Young Africans SC.
Mshery aliyejiunga na Young Africans kipindi cha usajili wa dirisha dogo msimu wa 2021-2022, yupo ndani ya mipango ya timu katika kuendelea kuboresha kikosi chetu kuelekea msimu ujao wa 2024-2025.
Kipa huyo ambaye ni mtulivu anapokuwa golini kulinda nyavu zake zisitikiswe, amekuwa mbadala sahihi wa Djigui Diarra pindi anapokosekana.
Msimu uliopita kipindi cha michuano ya AFCON wakati Diarra alipokuwa na majukumu ya kuitumikia Timu ya Taifa ya Mali, Mshery alisimama imara langoni na kuendelea kuifanya timu kubaki kwenye mstari wa kutetea ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC na tukafanikiwa.
Katika kipindi cha misimu miwili na nusu aliyokuwa ndani ya Young Africans SC, Mshery ameshinda ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC mara tatu, Kombe la FA mara tatu na moja Ngao ya Jamii.