Mtangazaji wa zamani wa Redio Tanzania Dar Es Salaam aliyekuwa akiripoti kutokea Zanzibar, Yusuf Omary Chunda, alikuwa na msemo wake maarufu wa kiarabu wa "Man Jitahada wa Jadda", kwa Kiswahili, "Mwenye Kujitahidi Hupata'.
Kila alipokuwa akiripoti kutoka Zanzibar, ilikuwa lazima atafute sehemu ya kuuweka msemo huu.
Kimsingi alikuwa akijenga moyo wa kutokata tamaa kwa wasikilizaji wake.
Huo moyo wa kutokata tamaa ndiyo umeisadia Morocco kupata nafasi ya kuandaa Kombe la Dunia la Soka la mwaka 2030.
FIFA imetangaza kwamba katika kusherehekea miaka 100 ya Kombe la Dunia, mashindano ya mwaka huo yatafanyika katika nchi sita za mabara yote, ikiwemo Morocco kutoka bara la Afrika.
Morocco ilianza harakati za kuomba kuandaa Kombe la Dunia la 1994, ikashindwa na Marekani.
Ikaomba kuandaa 1998 lakini ikashindwa ma Ufaransa.
Ikaomba kuandaa 2006, ikashindwa ma Ujerumani.
Ikaomba kuandaa 2010, ikashindwa na Afrika Kusini.
Ikaomba tena kuandaa 2026, ikashindwa na mataifa maratu yatakayoandaa kwaa pamoja; Marekani, Mexico ma Canada.
Lakini safari hii maombi yao ya kuandaa Kombe la Dunia la 2030 yamekubaliwa na hatimaye Morocco wamekipata walichokuwa wakikitafuta kwa miaka mingi.
Man Jitahada wa Jadda... Mwenye Kujitahidi Hupata!