Baada ya kuanza Ligi kwa kusua sua tofauti na ilivyomaliza msimu uliopita ambapo waliibuka mabingwa wa Ligi Kuu 2020/2021 na kubeba kombe la Azam Sports Federation.
Mpaka sasa Simba wako nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi wakiwa na alama 11 nyuma ya vinara Yanga wenye alama 15 huku kila timu ikiwa imeshacheza michezo mitano.
Sasa kiungo Mshambuliaji wa Simba, Bernard Morrison, amefunguka kuwa licha ya hali ngumu wanayokutana nayo mwanzoni mwa msimu huu, bado kikosi hicho kina nafasi kubwa ya kutetea ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu.
Simba, Jumatano iliyopita wakiwa katika Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam, walifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Namungo, na kufikisha pointi 11 katika nafasi ya pili nyuma ya Yanga wenye pointi 15, michezo sawa.
Akizungumza Morrison amesema: “Ni kweli hatujawa na matokeo mazuri katika michezo yetu iliyopita msimu huu kulinganisha na wapinzani wetu, lakini niwahakikishie kuwa bado tuna muda wa kubadilisha hili na kama wachezaji tunafanya kila jitihada kuhakikisha tunapambana kutetea kombe letu msimu huu licha ya upinzani mkubwa ambao tunatarajia kukutana nao kutoka kwa wapinzani wetu.”