Dar es Salaam. Kiungo wa Simba, Jonas Mkude amekosekana katika mazoezi ya timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ yaliyoanza jana Jumatatu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Taifa Stars imeanza mazoezi kujiandaa na mashindano ya CHAN 2020 yanayotarajiwa kufanyika Cameroon Aprili huku Tanzania ikiwa Kundi D pamoja na Zambia, Namibia na Guinea.
Katika mazoezi hayo wachezaji wote wa Simba walikuwepo isipokuwa Mkude pekee ambaye haikufahamika alikuwa wapi.
Kocha mkuu wa Taifa Stars, Etienne Ndayiragije amesema hawezi kuzungumza chochote kuhusu Mkude kwa kuwa hana taarifa rasmi za kuchelewa kwake kambini.
Meneja wa Stars, Nadir Haroub 'Cannavaro' amesema hawana taarifa ya kukosekana kwa Mkude kambini.
"Sina taarifa naye ila tu amechelewa na wewe haumuoni hapa, tumeingia kambini tangu tarehe 12 na yeye hajaripoti," alisema Cannavaro.
Pia Soma
- Mzee Yusuf apata kigugumizi kufafanua ‘Narudi Mjini’
- KIMENUKA JANGWANI: Molinga ana siku 3 tu Yanga
- Ndoto za Miraji Athuman zakatishwa kikatili Simba
Mara kwa mara kiungo huyu (Mkude) amekuwa akishindwa kufika kwa wakati katika kambi ya timu ya Taifa Tanzania.
Wachezaji wa Simba waliopo kambini ni Aishi Manula, John Bocco, Mohamed Hussein, Hassan Dilunga na Shomari Kapombe.