Timu ya soka ya taifa, Harambee Stars, ambayo haijacheza mechi yoyote ya kimataifa tangu kufungiwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) mapema mwaka huu, imepanda nafasi moja katika viwango vya ubora wa soka vinavyotolewa na FIFA kutoka 102 hadi 101.
Kwasasa Kenya inatumikia adhabu ya kufungiwa kwa muda usiojulikana na FIFA kufuatilia uamuzi wa Serikali kuingilia usimamizi wa shughuli za soka Novemba mwaka jana.
Mara ya mwisho Harambee Stars kucheza mechi ya kimataifa ilikuwa Novemba mwaka jana ilipoifunga Rwanda mabao 2-1 katika mechi ya kufuzu Kombe la Afrika.
Katika orodha ya 10 bora duniani kuelekea Kombe la Dunia, Brazil bado wapo kileleni ikifuatiwa na Ubelgiji, Argentina, Ufaransa, England, Italia, Hispania, Uholanzi, Ureno na Denmark.
Senegal ni baba lao Afrika ikiorodheshwa nafasi ya 18 duniani wakifuatiwa na Morocco, Tunisia, Nigeria, Algeria, Misri, Cameroon, Mali, Ivory Coast na Burkina Faso ambao wanafunga 10 bora za Afrika.