Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mikoa saba kukumbwa kimbunga 'Hidaya'

Hidaya Kimbunga Mikoa saba kukumbwa kimbunga 'Hidaya'

Fri, 3 May 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mikoa saba nchini inatarajiwa kuathirika na kimbunga ‘Hidaya’ kilichotarajiwa kusogea pwani ya Tanzania kuanzia usiku wa kuamkia leo.

Mikoa inayotarajiwa kupata athari ya mvua kubwa kutokana na kimbunga hicho ni Dar es Salaam, Mtwara, Lindi, Tanga, Pwani, Pemba, Unguja na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Morogoro.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) iliyotolewa, mgandamizo mdogo wa hewa umezidi kuimarika zaidi na mpaka kufikia jana tayari kimbunga Hidaya kilikuwa kilomita 506 kutoka Pwani ya Mkoa wa Mtwara.

"Jana (juzi) tulitoa taarifa ya kuwapo kwa mgandamizo mdogo wa hali ya hewa karibu na pwani ya mkoa wa Mtwara, mgandamizo huo imezidi kuimarika na kutengeneza kimbunga Hidaya ambapo kinatarajiwa kufika kwenye Pwani ya nchi yetu usiku wa kuamkia kesho (leo)," imesema taarifa ya jana ya TMA.

Hali hiyo ya kuwapo kwa kimbunga Hidaya kutasababisha upepo mkali na mvua kubwa hususani leo kwenye mikoa ya Lindi na Mtwara na kusambaa kwenye maeneo mengine ya pwani ya Tanzania kufikia kesho.

"Wananchi wote wanaofanya shughuli zao baharini wanashauriwa kuchukua tahadhari na pia kufuatilia taarifa za tahadhari kutoka TMA," imesema taarifa hiyo.

Aidha, Mamlaka hiyo imewataka wananchi kufanyia kazi ushauri wa kitaalam kutoka kwa sekta husika kuhusu athari hizo. Hali ya kimbunga na mvua kubwa kunatarajiwa kuanza kupungua Mei 6, mwaka huu.

Taarifa hiyo ya TMA imekuja huku baadhi ya maeneo ya nchi yakiendelea kukumbana na athari ya mvua kubwa inayoendelea kunyesha nchini.

Baadhi ya mikoa mbalimbali hapa nchini imeathirika na mvua ikiwamo mikoa ya Dar es Salaam, Lindi, Mtwara na Zanzibar na kuharibu miundombinu na makazi ya watu.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live